Facebook

Monday 12 May 2014

Lugola:Serikali ya CCM inaendeshwa kisanii


Mbunge machachari wa Mwibara, Alphaxard Kangi Lugola, amedai kuwa Serikali ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ambayo yeye ni mbunge wake, inaendeshwa kisanii.


Lugola ambaye katika Bunge lililopita aliwaongoza wabunge wenzake kuichachafya Serikali hadi mawaziri wanne kujiuzulu nyadhifa zao, jana aligeuka tena mwiba kwa Serikali ya CCM.

Akichangia hotuba ya Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika, Lugola alisema anashangaa Waziri mwenye dhamana, Christopher Chizza kuendelea kuwa waziri wakati hotuba yake imejaa blabla.

Pia alimgeukia naibu wa wizara hiyo, Godfrey Zambi na kumwambia kuwa amejisahau kwamba naye alikuwa akikaa kiti cha nyuma bungeni akipaza sauti, lakini baada ya kupata madaraka amewageuka na kushirikiana na waziri.

Akichangia kwa hisia kali, Lugola alihoji inakuwaje wakulima wanapelekewa pembejeo feki, dawa feki na skimu za umwagiliaji zinachakachuliwa na bado Chizza anaendelea kubaki ofisini kama Waziri.

“Waziri huyuhuyu ndiye anayezindua mbegu aina ya Chutoni ambayo haioti, bado ni Waziri. Waziri huyu huyu analipa ruzuku mbegu ya pamba isiyoota bado ni Waziri,” alisema Lugola.

Lugola alihoji kama Mchina aliyekuwa akijenga daraja la Kilombero alijiua kwa sababu tu ya kuhofia kupigwa risasi atakaporudi kwao, hata Waziri Chizza alipaswa awe ameiacha kazi hiyo.

“Simshauri waziri ajiue, lakini kwa vitendo vyote hivi waziri huyu angekuwa ameacha wizara hii na kupumzika na kufanya kazi nyingine mbadala,” alisema Lugola huku akipigiwa makofi.

Lugola alikumbushia Chizza alikuwa ni miongoni mwa mawaziri waliotajwa kuwa ni mizigo na kusema mambo yanayofanywa na wizara hiyo yatakigharimu Chama Cha Mapinduzi.

Mbunge huyo alibainisha kuwa, katika hotuba yake mwaka jana, Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, alisema Serikali iko kwenye mchakato wa kuanzisha mfuko wa kinga ya pamba ili kuwasaidia wakulima.

Hata hivyo, alisema katika hotuba ya Waziri Mkuu juzi, hakuna sehemu aliyozungumzia mfuko huo wala Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika katika hotuba yake ya mwaka huu, naye hajazungumzia mfuko huo.

“Hivi nchi hii tunaiendesha kwa usanii mpaka lini? Usanii juu ya usanii… Hatuwezi kuwadanganya wananchi kwa kiwango hiki. Itakuwaje mimi mbunge niunge mkono bajeti ya namna hii?” alihoji.

0 comments:

Post a Comment