Facebook

Wednesday 11 November 2015

NINACHOAMINI MAESTRO:-GEGENPRESSING KUTOKA KWA SUPER JURGEN KLOPP.

Na: Ayoub Hinjo(Ayo's Mata Maestro)

Mafanikio yoyote huja baada ya kuwa na mipango thabiti ndani yake,kamwe huwezi kuwa kwenye mafanikio kama hutakuwa na mipango iliyonyooka na yenye msimamo ndani yake. Uthabiti wa mipango yako,ndio mafanikio yenyewe kwako. Kuelekea kwenye mafanikio kila mtu huja au hutafakari mbinu zake ambazo anaamini zitamuweka kwenye kilele cha mafanikio yake. Ndivyo maisha yetu yalivyo kwenye dunia hii.

Mafanikio ya timu yoyote huja kutokana na mbinu za kocha na aina ya wachezaji ambao yuko nao kwenye timu pamoja na urafiki bora wa kazi ambao watautengeneza baina yao. Mbinu chanya za kocha huleta mafanikio zaidi kwenye timu na mwishowe huweza kushinda zawadi ambayo walikuwa wanaipigania. Mipango na mbinu za kocha mara nyingi hutegemea na aina ya wachezaji ambao yuko nao kwenye timu yake. Siku za karibuni tulishuhudia Jose Mourinho akimuuza mchezaji bora wa timu kwa misimu miwili mfululizo huku akisisitiza hayupo ndani ya mipango yake kwenye timu.

Miaka ya hivi karibuni tumeshuhudia makocha mbalimbali wakija na mbinu zao ambazo wanaamini zitaleta matunda kwenye timu zao. Kati ya makocha hao kuna kocha mmoja anaitwa Jurgen Klopp ambaye amekuja na mfumo unaoitwa Gegenpressing.

Gegenpressing ni nini!? Nafikiri hilo ndio swali ambalo utakuwa unajiuliza. Gegenpressing ni mfumo ambao kazi yake ni kufanya mashambulizi ya kushtukiza kwa presha ya ajabu au haraka kwa wapinzani. Mfumo huo huibana timu pinzani na kuifanya washindwe kucheza kama walivyozoea sababu wanalazimishwa kufata mapigo ya mfumo huo,pia kwa mfumo huo hufanya uwanja kuonekana mdogo kwa wapinzani sababu njia au nafasi ambazo mpira hutakiwa kupita zinakuwa zimefungwa. Msingi wa mfumo huo ni vitu viwili vikuu ambavyo 1. Stamina ambayo humfanya mchezaji husika kucheza kwa dakika zote bila kuchoka kwa kasi ya haraka ya kushambulia au kuzuia. 2. Uwezo wa kila mchezaji mmoja mmoja wa kufanya marking au tackling na timu kuhimili msukumo wa presha ambayo wapinzani wanayo. Mara nyingi mfumo huo huonekana pale timu inapokwenda kushambulia sababu kasi ya mashambulizi hutokea pale wapinzani wanapopoteza mpira na kushindwa kurudi kwenye nafasi zao kwa haraka.

Kocha wa Bayern Munich,Jupp Heynckes aliiwezesha timu hiyo kushinda makombe makubwa matatu mwaka 2013 kwa staili hiyo ya Gegenpressing. Staili hio ndio iliifanyia mauaji ya kutisha Barcelona kwa magoli 7-0 na Borrusia Dortmund kwa magoli 2-1 kwenye fainali ya klabu bingwa Ulaya mwaka 2013. Mfumo huo umekuwa maarufu sana kwa sasa na baadhi ya timu za Ujerumani na Hispania wakuwa wateja wakubwa wa mfumo huo pia hata timu ya taifa ya Ujerumani wamekuwa wakiutumia kwa sasa.

Gegenpressing. Asante sana Jurgen Klopp kwa kutuletea hiki kitu. Japo Pep Guardiola naye ametuletea Tik-Tak(Nipe Nikupe) kwenye uso wa dunia yetu ya soka.

0 comments:

Post a Comment