Facebook

Wednesday 23 July 2014

Chelsea walipomkaba mchezaji mnene zaidi duniani

 
JUMAMOSI jioni, John Terry aliwaongoza mabeki wa Chelsea kukabiliana na mchezaji mnene na mwenye nguvu zaidi duniani, Saheed Adebayo Akinfenwa ambaye umbo lake linaleta kichekesho kikubwa kwa mashabiki wa soka.
Chelsea ilishinda mabao 3-2 wakati huu ikijiandaa na michuano mbalimbali msimu ujao, lakini walilazimika kukabiliana na Akinfenwa ambaye alikuwa katika ubora wake.
Hadi wakati anatolewa uwanjani dakika ya 60, Chelsea ilikuwa imekufa 2-0 huku Akinfenwa akimuhenyesha Terry na wenzake. Hata hivyo baadaye walifunga mabao matatu ya haraka haraka yaliyobadili matokeo ya mechi wakati Akinfenwa akiwa nje ya uwanja.
Licha ya umbo lake kubwa, Akinfenwa aliyezaliwa jijini London Mei 10, 1982 anadaiwa kuwa na kilo 86 tu lakini ana uwezo wa kubeba uzito wa kilo 180 ambazo ni mara mbili na uzito wake.
Tayari Fifa wamempitisha kama mchezaji mwenye nguvu zaidi duniani huku wakimuingiza katika Video zao za michezo ya kompyuta huku umbo lake likionekana kuwa kivutio kwa mashabiki wengi duniani.
Mlinzi wa klabu ya Vale iliyo daraja la kwanza England ambaye alicheza timu moja na Akinfenwa Northampton, Dan Jones anaeleza kwamba ni kujisumbua tu kujaribu kutumia nguvu kumkaba mchezaji huyo.
“Soka lake halibadiliki tangu tulipokuwa Northampton. Anapenda kuuficha mpira miguuni na inajionyesha wazi kwamba hana mpango wa kukimbia nao. Anapenda kukaa na mpira mguuni huku akiwasukuma walinzi kwa nguvu zake.” Anasema Jones.
“Hauwezi kushindana naye kwa nguvu kwa sababu utaishia kumfanyia rafu au atakutupa tu. Inabidi utumie akili sana wakati wa kumkaba. Inabidi usitumie nguvu nyingi sana kumkaba.”
“Wakati mwingine akipata mpira tunamuachia tu na kuangalia anachotaka kufanya kwa sababu tunajua hawezi kukimbia, yeye huwa anaaangalia watu wanaofungua nafasi tu.” Anasema Jones.
Akinfenwa amedai kwamba hajawahi kucheza katika Ligi Kuu ya England kwa sababu makocha wamekuwa wakiliogopa umbo lake na kudhani kwamba atakuwa mzigo tu uwanjani kitu ambacho sio cha kweli.
“Nadhani naweza kutisha Ligi Kuu. Nadhani niko sawa na Didier Drogba tu. Sijacheza madaraja ya juu kwa sababu kuna mtazamo fulani wa jinsi ambavyo mwanasoka anapaswa kuwa na mimi sionekani kuwa hivyo,” anasema Akinfenwa.
“Sitaki kuonekana mjinga lakini nimefunga zaidi ya mabao 150 katika mechi 300. Waulize walinzi au makocha wa timu pinzani watakwambia jinsi nilivyo balaa.” Anasema staa huyo.

0 comments:

Post a Comment