Facebook

Saturday 19 September 2015

CHADEMA wapanga kumshtaki Dr.John Magufuli kwa matumizi ya M4C

Dar es Salaam. Chama cha Chadema, kimesema kinakusudia kumfungulia mashtaka Dk John Magufuli kwa madai ya kutumia nembo yake ya ‘M4C Movement For Change’ ikiwa na maana “Vuguvugu la Mabadiliko” na kuigeuza kuwa ‘Magufuli for Change’ kwa muundo uleule.
Akiwa Kata ya Nguruka, Kigoma Kusini mkoani Kigoma, Jumatano wiki hii Dk Magufuli alisema maana ya neno M4C ni ‘Magufuli for Change’
“Wanasema M4C, mnajua maana yake?” aliuliza na kujibu mwenyewe. “Maana yake ni Magufuli for Change.”
Mwanasheria wa Chadema, John Malya alisema nembo hiyo ni mali ya Chadema na imesajiliwa kwa Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (Brela).
Alisema wameamua kumpeleka mahakamani ifikapo Septemba 21. “Dk Magufuli amekiuka sheria ya Trade and Service Mark Act ya mwaka 1986, kanuni za Trade and Service Mark Regulation ya mwaka 2000. Lakini pia na sheria ya hakimiliki ya dunia World Intellectual Property Organization Convention ya mwaka 1963 iliyofanyiwa marekebisho Tanzania mwaka 1983,” alisema Malya.
Mkuu wa Kitengo cha Habari Chadema, Tumaini Makene alisema baada ya Magufuli kuiteka wafuasi na wapambe wake wa kampeni walitengeneza nembo hiyo na kuanza kuitumia.
Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye alipoulizwa juu ya tuhuma hizo alisema, “Waache watangulie Mahamani. Tutakutana huko.”
Msajili wa Vyama vya Siasa, Jaji Francis Mutungi alipoulizwa alisema: “Sijapata malalamiko yoyote hivyo siwezi kusema chochote hadi watakapofanya hivyo.”
Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguz (NEC), Jaji Mstaafu, Damian Lubuva alisema, “Hatuhusiki na hatimiliki ya nembo wala sera."

CHANZO:MWANANCHI

0 comments:

Post a Comment