Facebook

Thursday 27 November 2014

UBORA WA EDEN HAZARD: HaKUNA LILILO SAWA KATIKA DUNIA HII ISIYO SAWA.

Kama Kuna swali gumu na lisilo na Jibu sahihi
miongoni mwa maswali mengi katika viwanja vya
soka basi ni lile linalohusisha neno kipaji. Kila
nikimtizama Angel Di Maria Kisha nikatupa jicho
mahala alipo Downing baadae nikamtizama Yaya
Toure Kisha nikaona anachofanya Lucas roho inauma
zaidi. Hata hivyo ndio soka, linakupa Majibu na
maswali tofauti. Wakati unawaza uwezo wa Yaya
Toure unajiuliza ni vipi anadhibitiwa vilivyo na yule
Charlie Adam wa Stoke City wakati katika karatasi
hafiki nusu ya uwezo wake? Ndio maana Siwezi
kumshangaa James Pinkerton alivyyowahi kusema
kuwa HAKUNA LILILO SAWA KATIKA HII DUNIA
AMBAYO HAIPO SAWA. Alikuwa sahihi zaidi, dunia
haipo sawa, watu hatupo sawa hata vipawa havipo
sawa pia.

Bahati mbaya tu hatuna namna Mara
nyingine inabidi uviweke visivyo sawa vifanye kitu
kimoja. Ni kama kushudia Messi na Sanogo wakiwa
watu wa nafasi moja uwanjani katika timu kubwa
mbili tofauti.

Umewaza Ubingwa wa Premier League msimu huu?
Kwakua dunia haipo sawa kama James Pinkerton
alivyosema si ajabu hata mashabiki wa Liverpool
baadhi wapo ambao bado wanaofikiria na kuamini
kuwa wanaweza kupata ubingwa. Ingawa kwa wale
wanaoshika kalamu na karatasi vyema wana imani
Mourinho anayo nafasi kubwa zaidi ya mtu yeyote,
unahitaji roho ya Daudi yule wa Goliath kulipinga hili
yaani roho ngumu na ya kijasiri kweli. Nipo nauwaza
ubingwa wa Chelsea, lakini kwa namna tofauti kidogo.

Najiuliza kama ikitokea nani atatizamwa kama
mfalme? Nani ataimbwa Sana pale Stamford bridge?
Nani atayarithi yale mabango mazuri ya Super
Frankie Lampard kule jukwaani? Baadae nawaza nani
atakuwa kipenzi cha Abramovich? Hapana shaka wa
kwanza atakuwa Mourinho mwenyewe, na kwa
ubinadamu mwingine atakuwa Diego Costa Kisha
Cesc Fabregas. Kuna Tatizo hapa, yule fundi wao
Eden Hazard sio ajabu akawa nyuma ya Nemanja
Matic. Unajua kwanini? Sitoshangaa Sana ikitokea
hivyo na Jibu ni rahisi tu, dunia haipo sawa kwa kiasi
kikubwa hivyo na Hazard hajakaa sawa. Kwa lugha
ya kitaalamu katika soka Hazard anakosa kitu
kinaitwa FOOTBALL MATURITY, yaani anakosa
ukomavu wa soka.

Ukomavu unaanzia katika
uwezo,Kisha malengo baadae maamuzi. Hapa akili
inabidi iwe imeiva kweli. Hazard ana uwezo, malengo
lakini analo tatizo la maamuzi. Maamuzi yake huwa
sahihi Sana pale anapopiga penalti kuliko anapokuwa
anamiliki mpira ndani ya uwanja. Na hii ndio sababu
inayomweka nyuma ya wachezaji wengi katika
mtiririko wa heshima, tuzo na ubora.
Hakuna uhalisia wowote wa uwezo wa Sterling juu ya
Hazard, usiwaze kuhusu Mata dhidi ya Hazard, kama
ni kipaji Hazard anawekwa ukurasa mmoja na Angel
Di Maria. Na pengine ndio mchezaji mwenye mbinu
nyingi zaidi na umaridadi wa kipekee awapo uwanjani
kuliko mchezaji mwingine yoyote Ligi ya Uingereza.

Lakini anao huo ugonjwa tu unaoitwa ukomavu. Kwa
mchezaji Kuna umri ukifika ama kipindi kikifika
unaacha baadhi ya mambo na kufanya vile vitu vya
msingi zaidi, unaacha kupiga chenga wachezaji
wanne, unaacha kukimbizana na mpira kwenye msitu
wa watu kwa sekunde 50, unapunguza mchezo wa
kwenye kioo ule wa Adnan Januzaj, huu ni mchezo
wa makinda bora wanaochipukia katika kuvutia
wawekezaji ambao ni timu kubwa.

Katika kipindi hiki
we unajifunza na unajikita katika kujiweka katika
nafasi sahihi na katika muda sahih. Unaacha
kupigana vikumbo na akina Shawcross au Koscielny
unajifunza kucheza pembeni mwa mabega Yao.
Maana yake kwa lugha nyepesi unaanza kujifunza
kucheza na kipa na sio mabeki yaani ujifunze
kufunga, Hazard Ana shida hapa, anaumwa hapa na
amelala hapa. Hazard analo tatizo la kutoweza kuwa
muhimili wa awali kabisa wa timu, atakupa kile
unachotaka kama tu Kuna mtu mwingine wa kufanya
baadhi ya majukumu ambayo kimsingi alitakiwa
ayafanye yeye.

Kwa Hilo huwezi shangaa kwanini
Juan Mata aliweza kuwa mchezaji bora Mara mbili
wa chelsea mbele yake. Kwa hilo hapana shaka
Chelsea wangeweza kuwa mabingwa msimu uliopita
kama wangekuwa na nguzo nyingine pembeni yake
achilia mbali tuzo ya mchezaji bora anayechipukia
aliyopewa ambayo ninaamini kwake ilichelewa na
alitakiwa kuipata misimu miwili nyuma.

Soka la sasa
linampa ugumu Hazard, mbio, chenga, na Kanzu na
magoli machache na assist kiasi haviwezi kukupa
Ballon D'or katika Ulimwengu huu ambao Diego Costa
na Suarez wanafunga goli 30 peke Yao, katika dunia
hii ambayo wachezaji wa pembeni wenye uwezo
wanatakiwa kufunga kwa kiasi kikubwa. Hapa ndipo
mabadiliko yake yanatakiwa. Kwa wachezaji wa
kariba yake unahitaji uwezo mkubwa wa kufunga ili
uwe na uelekeo wa kuwa Mchezaji bora wa dunia.
Roho inaniuma maana naona mwenye uelekeo huo
katika kundi la kina Hazard ni Neymar.

Huyu ndio
anayekomaa vizuri pamoja na akina Bale na James
Rodriguez. Hata Ubelgji walishindwa hapa,
alichotakiwa kufanya Hazard alikifanya De Bryune,
mchezaji tusiemfikiria huko juu. Dunia haipo sawa
kweli, ndio maana Hazard anaiwaza Ballon D'Or
pasipo kubadili maamuzi. Sio maamuzi mengine Bali
ni yale maamuzi unapokuwa mbele ya goli. AJUE
KUFUNGA TU. Vinginevyo tutaendelea kumsujudia
Alexis Sanchez kama mchezaji wa Pluto. Mi kwangu
Hazard bado mtoto sijui kwako wewe, ila mi naamini
hajakomaa.

Acha niwaze kuwa atabadilika,ingawa
ananipa wasiwasi kama ataweza kuwa mshindi wa
Ballon D'OR , anaweza hasibadilike si unajua hakuna
lililo sawa katika dunia hii isiyo sawa na ndio maana
wengine tunaenda mbali na kumfananisha na Ronaldo
Cristian huwa natamani kulia lakini nahairisha kila
nikimkumbuka James Pinkerton, kweli hakuna lililo
sawa katika dunia hii isiyo sawa lakini natamani
kuiona suti ya Hazard miaka fulani akiwa miongoni
mwa watatu wanaotakiwa kushinda Ballon D' Or.
Ahsanteni

0 comments:

Post a Comment