Facebook

Friday 27 June 2014

Magaidi wajifaidisha na uwindaji haramu

moja wa Ndovu waliouawa na wawindaji haramu nchini Kenya
Makundi ya kigaidi na wanamgambo wamekuwa wakifaidi kutokana na uwindaji haramu wenye thamani ya dola bilioni 213 kila mwaka, na kutishia usalama wa kimataifa.
Hii ni kwa mujibu wa ripoti mpya ya shirika la UNEP.
Ripoti hiyo ilizinduliwa katika kongamano la kwanza kabisa la umoja wa Mataifa kuhusu mazingira lililoandaliwa nchini Kenya
Kwa mujibu wa ripoti hiyo, kundi la Al Shabab nchini Somalia hupata kati ya dola milioni 38 na 56 kila mwaka kutokana na biashara haramu ya uuzaji makaa.
Kwa jumla, makundi ya wanamgambo na kigaidi yaliyoko barani Afrika, yalipata kati ya dola milioni 111 na 289 kila mwaka kwa kujishughulisha na kutoza ushuru na uuzaji haramu wa makaa.
“makundi mengine yanayonufaika na biashara haramu ya wanyama pori , yalijipatia kati ya dola milioni 4 na 12.2 kila mwaka kutokana na uuzaji wa pembe za ndovu katika eneo la Afrika ya Kati,.
'Athari kwa hesabu ya Ndovu'
Pembe za Ndovu zimekuwa zikinaswa kila kukicha katika kanda ya Afrika Mashariki
Uhalifu huu pia ulichangia pakubwa katika kupunguka kwa idadi ya ndovu barani Afrika,” ripoti hiyo ilisema.
Ripoti hiyo inajiri siku chache tuu baada ya kushuhudia uharibifu mkubwa wa mazingira katika mbuga ya wanyama ya Tsavo Mashariki.
 Ilionekana mizoga ya ndovu waliouwawa hivi majuzi huku Kenya kwa mara nyingine tena ikipoteza ndovu wake wanaoleta mapato mengi ya kitalii.
Mwandishi mmoja anasema uvundo kutoka mzoga wa ndovu wa miaka thelathini ulifuka kutoka umbali wa mita kadhaa kutoka eneo alipofariki Ndovu huyo baada ya kuuwawa na wawindaji haramu
“Ndovu huyu alikuwa katika kundi la wengine watatu, na alipigwa risasi kutumia bunduki ya rashasha na pembe zake kukatwa.
Mkaa ambao umekuwa ukiuzwa kimagendo na kundi la Al Shabaab
Tazama uso wake ulivyoharibiwa vibaya kwa kukatwakatwa,” alitueleza afisa mmoja anayelinda mbuga ya kibinafsi katikati kabisa ya Mbuga za Tsavo Mashariki na Magharibi.
Karibu na eneo hilo kulikuwa na alama nyingi nyeusi ardhini. Hii ilikuwa damu ya ndovu wengine wawili waliouwawa. Damu hiyo ilikuwa imekaukia ardhini na kubadili rangi kutokana na jua kali katika eneo hilo.
Uwindaji haramu umekuwa tatizo sugu katika mbuga ya wanyama ya Tsavo kutokana na idadi kubwa ya ndovu katika eneo hilo. Hii imewavutia wawindaji haramu katika eneo hilo.
'Kazi kukabiliana na wawindaji haramu'
Ndovu na Vifaru wote wako katika hatari ya kuwindwa kiharamu
“ Mwaka jana tulipoteza zaidi ya ndovu sabini hapa, lakini mwaka huu pekee, tayari tumeandikisha vifo vya ndovu zaidi ya mia moja. Hatujui hata idadi kamili bado, ‘ alisema Dod Robson, mmiliki wa mbuga ya kibinafsi katika eneo la Tsavo.
Ripoti ya Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshugulikia masuala ya mazingira UNEP inasema katika kipindi cha miaka tisa, idadi ya ndovu imepungua kwa kasi kutokana na uwindaji haramu.
“Idadi ya ndovu wanaouwawa kila mwaka sasa ni kati ya 20,000 na 25,000 na hii ni katika idadi nzima ya kati ya ndovu 420,000 hadi 650,000, “ ilisema ripoti hiyo iliyonzinduliwa leo jijini Nairobi.
“ Pembe za ndovu zinazotokana na uwindaji haramu barani Afrika na kuuzwa barani Asia zinathamani ya kati ya dola milioni 165 na 188,” ripoti hiyo iliendelea kufafanua
Asilimia 94 ya uwindaji haramu wa Vifaru unatokea nchini Zimbabwe na Afrika Kusini, mataifa ambayo yana idadi kubwa zaidi ya Vifaru waliosalia duniani.

0 comments:

Post a Comment