Facebook

Thursday 15 May 2014

Madrid Wakubali Kuja Tanzania



REAL Madrid ya Hispania inatua nchini Agosti 21 ikiwa na nyota wake wa zamani.  Wachezaji kama Luis Figo, Ruud van Nistelrooy, Michael Owen, Zinedine Zidane watakuwemo kwenye kikosi hicho kilichopewa jina la Madrid Legend.
 
Ofisa Habari wa Kampuni ya TSN Limited ambao wanafanikisha ujio wa timu hiyo kubwa duniani, Dennis Ssebo alisema kuwa wachezaji Cristiano Ronaldo, Rameres na Iker Casillas watatengeneza matangazo ya ujio wa timu hiyo nchini.

“Jumamosi tutakuwa Lisbon kutengeneza matangazo ambayo yatarushwa Hispania na Tanzania kuhusu ujio wa timu hii, wachezaji hao mbali na kutengeneza matangazo pia tupo kwenye mazungumzo nao ikiwezekana nao wawe miongoni mwa wachezaji watakaokuja nchini,”alisema Ssebo.

Kikosi hicho kitakapokuwa nchini kitacheza mchezo mmoja wa kirafiki Agosti 23 na timu ambayo Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), itaiunda ambayo itajulikana kama Tanzania Eleven, mchezo utakaochezwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Real Madrid Legend kwenye mkutano huo iliwakilishwa na mkongwe na kapteni wa timu hiyo, Ruben de la Red aliyeambatana na Rayo Garcia pamoja na Isaac Recarey Sanchez anayehusika na mambo ya uhusiano ndani Madrid Legend Club. Walisaini mkataba wa ziara ya timu hiyo nchini na Mkurugenzi wa TSN Group, Farough Baghoza mbele ya waandishi wa habari katika mkutano uliofanyika kwenye ukumbi wa Serena jijini Dar es Salaam.

Ssebo alisema timu hiyo itawakilishwa na wachezaji 25 na watakaa nchini kwa siku tatu wakiwa na ratiba mbalimbali.

“Wachezaji hawa wakongwe ambao bado wako fiti na wanacheza wanatazamia kutembelea mbuga za wanyama, “alisema Sanchez.

Aliwashauri vijana wa timu ya Tanzania kujifua kwa kuwa yawezekana kikosi hicho cha Madrid kiko fiti. Rais wa TFF,  Jamal Malinzi alisema; “Ujio wa timu hii utatupa mafunzo mengi na uzoefu walionao wachezaji hawa lakini pia watasaidia kuitangaza nchi kwa ujumla.”

0 comments:

Post a Comment