Facebook

Sunday 21 September 2014

Moto wateketeza nyumba 21, Tufani yaezua 11, 240 wakosa makazi Sengerema

Wakazi 240 wanaoishi kisiwa cha Nyamango
kijiji cha Lushamba kata ya Buliaheke
Wilayani Sengerema hawana makazi ya kuishi
kutokana na kuzuka kwa moto usiku wa
septemba 19 na mvua iliyombana na tufani
mapema asubuhi ya jana(leo).

Mkuu wa Wilaya Sengerema Elianas Balangyo
alisema kuwa kamati ya maafa ilikuwa
haijafika katika eneo la tukio na ilikuwa
ikisubiri kutulia kwa mawimbi ziwani ili
kuanza safari ya kufika kisiwani hapo
kutathimini kiasi cha maafa kichotokea ili
kutoa msaada unaohitajika.

“Mpaka sasa hatujafika eneo la tukio
kutokana na kuwa eneo lililokumbwa na
matatizo hayo haliko nchi kavu hivyo
tunasubiri ziwa litulie ili kamati iende
kufanya tahimini na kupata kiasi cha msaada
kinachotakiwa kupelekwa na aina ya msaada
unaotakiwa pia” alisema DC. Balangyo.

Mwenyekiti wa kitongoji cha Nyamango
George Lwezaula alisema kuwa haijulikani
chanzo cha kuzuka kwa moto na kuwa
ulitokea saa 6.05 usiku katika nyumba moja
ya mkazi wa katika kitongoji hicho. Inadaiwa
kuwa moto huo ulitokana na familia hiyo
kusahau kuzima jiko baada ya kumaliza
kuandaa chakula na kuingia kulala na
kuchukuliwa na upepo na kushika nyumba
yake kisha nyumba nyingine.
“Nyumba 21 zimeungua na kuteketea kabisa,
ukizingatia kuwa vyumba hizi za wavuvi
zinajengwa karibu karibu lakini hakuna mtu
aliyedhurika licha ya mali zote kuungua
ndani” alisema Lwezaula Mwenyekiti wa
kitongoji cha Nyamango.

Hata hivyo alieleza kuwa asubuhi
mvua iliyoambatana na upepo mkali ilizuka
na kuezua nyumba 11 likiwemo kanisa la
Roman Katoliki na kufanya jumla ya nyumba
zilizoezuliwa na kuteketea kufikia 32. “Mvua
hii imeanza saa 1 asubuhi lakini ilikuwa na
upepo mkali ambao umebeba paa za nyumba
na kuacha wananchi wakiwa hawana pa
kujistili” alisema Lwezaula.
Mtendaji wa kata ya Buriaheke Mabula Enock
alisema taarifa hiyo aliipata kwa njia ya simu
na alikuwa Wilayani Sengerema kutafuta
usaidizi wa kamati ya maafa ya Wilaya kuona
ni jinsi gani wanatoa msaada kwa wakazi hao.

“Nilipata taarifa hiyo jana na kuutaarifu
uongozi wa Wilaya, hapa nipo nafuatilia
kuona kuwa wanaingia saa ngapi kisiwani ili
kutathimini” alisema Enock.

0 comments:

Post a Comment